Friday, 12 May 2017

PROMO 1 - JIRANI YANGU MCHAWI


".......Watu wakalibeba lile jeneza lililokuwa na mwili wa mwanangu huku wakipokezana baada ya kila kitambo kidogo. Hatimaye wakafika nalo makaburini, wakaliweka jeneza pembeni mwa kaburi lililokuwa limeshaandaliwa.Katekista aliongoza sala ya mazishi, kisha zoezi la kumzika mwanangu likafuata.Jeneza liliingizwa kaburini taratibu hadi likatua kwenye sakafu ya kaburi lile. Wakachota mchanga na kuniletea ili mimi niwe wa kwanza kutupa mchanga kaburini japo kiganja kimoja. Nikasisimuka mwili, taratibu nikachota ule mchanga nikaumimina taratibu kwenye kaburi la mwanangu Sostenes. Jinsi nilivyozidi kumimina ule mchanga ndivyo na machozi yalivyozidi kunitiririka na mengine kumiminika hadi ndani ya kaburi la mwanangu. Nilipomaliza nikaondoka taratibu ili kumpisha mke wangu naye amzike mwanaye. Haikuwa rahishi Mama salima kuchukua kiganja cha mchanga na kumimina kwenye kaburi la mwanae, basi wanawake Fulani walimshikilia na kumsaidia hadi akatupa mchanga ndani ya kaburi la mwanae. Akafuata Sabrina japo naye kwa kushikiliwa. Ndugu wengine wakafuata na baadaye wengine wakalishambulia kaburi la mwanangu kwa kutupia mchanga kwa kutumia spedi na kushindilia kwa visigino vyao. Mimi nikiwa nimesimama pembeni niliwaza moyoni mwangu, nikajaribu kukumbuka mwanangu, machozi yakaanza kutoka tena. Kaburi lilipojaa wakaanza kushindilia kwa mikono. Mama Salma, mama wa marehemu alilia kwa nguvu hadi nikamwonea huruma japo mimi mwenyewe nilishikwa na uchungu sana kumpoteza mwanangu.
Kisha tukaweka mataji kwenye kaburi la mwanangu, nilianza mimi akafata mama yake akafuata Sabrina dada yake na kisha wajomba, binamu, shangazi na ndugu wengine wakafuata. Mazishi yalipomalizika mtangazaji, mzee Ndeluvale akatangaza kuwa watu warudi nyumbani kwa wafiwa wakanawe mikono, akimaanisha wakale chakula. Basi watu wakaanza kurudi, mimi nilikawia kidogo, nilitamani kama nibaki kaburini lakini ilinilazimu niondoke.
Tulipofika nyumbani chakula kilikuwa kimeandaliwa, watu wakala wakashiba na kusaza. Mimi sikuweza kula mchana ule. Nilianza kufatilia kujua hali ya binti yangu Salma aliyekuwa amepoteza fahamu wakati wa kwenda kuaga maiti ya mdogo wake. Hali ya binti yangu ilikuwa shwari, nikatiwa matumaini.
Usiku watu waliobaki kukesha na kuomboleza pamoja nasi, walikuwa wakiimba nyimbo za aina nyingi. Baadhi ya nyimbo hizo nilikuwa nazifahamu na nyingine zilikuwa ngeni kabisa kwangu. Nyimbo nilizokuwa nazifahamu ni kama vile ule unaoitwa Twiwalala:
Uliimbwa hivi:
Moooja, mbili tatu twende twiwalala, (We twiwalala) x 2
Ve twiwalala umwanavesu(We twiwalala)
Umwana vesu asivoneha (We twiwalala)
Umwana vesu ahele hwina (We twiwalala)
Moooja, mbili tatu twende twiwalala, (We twiwalala) x 2
Pia waliimba ule wimbo wa“Parapanda italia,” pia na nyimbo nyingine nyingi zilizomtaja na marehemu mwanangu. Tulifarijika kwani watu waliguswa na kifo cha mwanetu hata wakashiriki nasi katika tukio hilo. Uliipoimbwa wimbo wa`twiwalala` sikusita kusimama na mimi kuimba. Kwa kawaida wimbo huu unapoimbwa kwenye msiba watu huanza kucheza kwa kuruka na kuzungukazunguka wakipapasapasa kama vile wanatafuta kitu kilichopotea na kwa wakati ule hakika ulikuwa ni wakati wa kumtafuta mwanangu Sostenes. Hivyo nilijumuika nao kupapasa kumtafuta mwanangu.
Tulicheza tukaruka tukiimba huku tukipiga yowe, huuuuwi, huuuuwi! Mara tukaanza kuondoka kuelekea makaburini. Akina mama fulani waliokuwa wanaimbisha walitangulia mbele, mimi nilikuwa katikati ya watu wengine, nami nilikuwa nikiimba kwa sauti kwani wimbo ule nilikuwa naufahamu vizuri na nilikuwa naupenda. Tukashuka ule mteremko mara tukakata kona, tukapitiliza vile vichaka vilivyo jirani na makaburi hatimaye tukaingia eneo la makaburini usiku ule huku tukiimba kwa sauti na kupiga yowe. Hapo sasa na mimi nikaharakisha nikawa mbele jirani na wale akina mama waliokuwa wanaimbisha. Kwa mbali niliweza kuona eneo ambalo tulimzika mwanangu. Tulivyozidi kusogea kwa mbali niliona kama kitu cheusi mfano wa kifurushi kikitoweka kutoka pale lilipo kaburi la mwanangu. Nilishituka ghafla nywele zikasimama, mapigo ya moyo yalienda kwa kasi, moyo ukadunda duf-duf-duf kijasho chembamba kikaanza kunitoka.

__________inaendelea_______
RIWAYA: KUMBE JIRANI YANGU MCHAWI
MTUNZI: ELIAS K. MWALONGO
SIMU: +255769313224
E-MAIL: mwalongoelias7@gmail.com


~~~MPENDWA MSOMAJI~~~
Nendelea kukuonjesha tu vipande vya Riwaya hii maridadi. Kitabu cha Riwaya hii ya kusisimua kinapatikana kwa tsh. 5000/-Tu.
Lakini pia KANTON PRINTING inakukaribisha kuwa dalali wa KITABU hiki popote ulipo ndani ya Tanzania, endapo uko tayari basi, utauziwa vitabu vya jumla kwa Tsh. 2500/-kila kimoja nawe utaenda kuuza kwa tsh.5000/-kama ilivyokwishaonyeshwa kwenye kitabu hicho. Endapo utakuwa tayari kuwa dalali basi itakupasa kuchukua walau kuanzia vitabu 20 na kuendelea. Ambapo vitabu 20 utachukua kwa tsh.50,000/- wewe utaenda kuuza kwa tsh.5000/-kila kimoja na kupata sh.100,000/-
Kwa maelezo zaidi wasiliana na mtunzi wa Riwaya hii No. +255769313224

Asante na Ubarikiwe mno!

NITAKUPENDA DAIMA

Mtunzi: Elias Kalistus Mwalongo Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Ruaha(RUCU) Simu: 0769313224 ____________ Laazizi wangu wa moyo, nat...