DADA`NGU
MCHUMBA`NGU
________________________________________________________________
Mtunzi: Elias K. Mwalongo(Kanton)
Ruaha Catholic UNiversity(RUCU)
+255769313224
Umri wangu si
haba, ni miaka ya kutosha kuitwa mtu mzima. Hata nikimwambia mtu yeyote kuwa nataka
kutafuta jiko hatanishangaa. Hata hivyo sasa nimechanganyikiwa akili, kichwani
ni maluweluwe matupu. Najaribu kulala ili nipoteze mawazo lakini usingizi
ukiisha mawazo yanarudia yaleyale. Ningekuwa mnywaji mzuri wa pombe, basi
ningenunua pombe ya kutosha hata viroba vingi au mvinyo, ili ninywe nilewe hata
nikizidiwa hadi kufa wacha nijifie tu.
Ninaikumbuka
siku ile ya jumamosi nilipomwendea baba yangu aliyekuwa amekaa sebuleni
akiangalia TV na nikamwambia kuwa nimepata mchumba na ninampango wa kumwoa
endapo wazazi na ndugu wangeridhia.
Nilimweleza
wazi baba yangu kuwa nilipata mchumba aitwaye Frida binti wa mzee Lukengelo.
Baba alishituka akanikodolea macho, akanisogelea akaongea kwa kuninong`oneza
akasema, “Mwanangu, umri wako unakuruhusu kuoa, umeshakuwa mtu mzima mwanangu,
lakini chonde nakuomba usimuoe Frida maana, yule ni dada yako kabisa na baba
yenu ni mimi ila naomba mwanangu usimwambie mama yako maana yeye hajui.”
Nilimkodolea macho baba, Nilitaka kubishia lakini yeye akaendelea, “mwanangu chonde
naomba utafute mwingine lakini usimwoe Frida maana ni dada yako na baba yenu ni
mimi ila naomba usimwambie mama yako maana yeye bado haelewi hilo.”
Nilifedheheka
na kuhuzunika moyoni kusikia kauli ya baba yangu. Kilichoniumiza zaidi ni ile
kauli ya kwamba nitafute mwingine nisimwoe Frida, ukizingatia ni binti pekee
ambaye nilimpenda kwa dhati, nilimweka moyoni mwangu. Alinipenda nami
nilimpenda kwa dhati, mawazo yangu muda wote yalikuwa ni kwake. Nilimpenda sana
Frida, yeye ndiye alikuwa ni shibe ya nafsi yangu na faraja ya moyo wangu.
Kumkosa Frida maishani mwangu nilihisi ni sawa na kupoteza kiungo kikubwa
mwilini mwangu.
Masaa yalienda
kwa kasi, siku zikaja na kupita wiki ya kwanza ikapita. Wiki ya pili nayo
ikabisha hodi na kunikuta ningali nafurukuta moyoni kwa hofu ya kumkosa Frida
maishani mwangu. Msongo wa mawazo ukanikondesha na kunifanya mnyonge kila muda.
Lakini ikafika wakati nikaona uvumilivu umenishinda, nisingeweza kuendelea
kuficha siri ambayo baba aliniambia. Nilihisi kabisa mpango wangu wa kufunga
ndoa na Frida ulikuwa umegonga mwamba. Basi niliamua liwalo na liwe, wacha
niyatoe ya moyoni. Niliamua nimwambie Mama ukweli wote ambao baba alinieleza na
kunisihi nisimwambie mama ili lisitokee timbwili lolote pale nyumbani. Kumbuka,
msiri wa siri ya moyoni ni mwanasiri mwenyewe. Msiri huiweka siri sirini mwake
na pango la siri ni moyo. Moyo wenyewe umeumbwa kisirisiri, hata ukiupasua,
kamwe hauwezi kukwambia siri ya msiri. Na siri ni siri kwa upande mmoja tu wa
mwanasiri, lakini ikishafahamika na wengine hiyo si siri tena. Na hii siri ya
baba haikuwa siri tena maana aliniambia mimi, nami nikashindwa kuihifadhi
moyoni nikaamua kumwambia mama yangu ili tu kutua mzigo mkubwa niliokuwa
nimeubeba moyoni mwangu.
Ni juzi tu
nilimfuata mama jikoni na kumkuta akijishughulisha na mapishi kama kawaida
yake. Nikamsalimu kwa heshima aliyonifundisha yeye mwenyewe, kisha nikatulia.
Yamkini mama aligundua kuwa nilikuwa na neno la kusema. Akanihamasisha niseme
shida yangu, nami nikaanza kusema maana ilikuwa ni shida kweli niliyokuwa nayo.
Nikamwambia, “Mama mimi nina neno la kusema” akadakia, “ehee sema mwanangu
nakusikiliza” Nikaendelea “ Mama mimi nimepata mchumba…” Kabla sijaendelea mama
aliweka bakuli lake chini alilokuwa amelishika, akakaa makini kunisikiliza
mimi. Nami nikaamua kuanza upya nikasema, “Mama mimi nimepata mchumba, mchumba
wangu anaitwa Frida, binti wa mzee Lukengelo, bila shaka unamfahamu! Mama
akasema, “ndio, namfahamu vizuri mzee Lukengelo na familia yake yote na huyo
binti uliyemtaja namfahamu. Mwanangu umri wako unakuruhusu, mimi naona umefanya
uamuzi mzuri. Jipange mwangu, nitamwambia baba yako na sisi wazazi wako
tutajipanga vema” Mimi nilikuwa namwangalia tu usoni anavonifagilia, kisha
nikasema, “Lakini mama, nimemwambia baba juu ya suala hili amenikataza kabisa
nisimwoe Frida, anasema kuwa Frida ni dada yangu na yeye ndiye baba yetu, ila
alinionya nisithubutu kukwambia wewe, nami nimevumilia kwa muda mrefu,
nimeshindwa kuendelea kuyaweka moyoni..” Niliongea maneno haya kwa hofu
nikiogopa timbwili litakalotokea pale.
Hata hivyo
nilimwona mama`ngu akitabasamu kwa furaha. Niliponyamaza kuongea akacheka
mamangu kwa furaha, akacheza na kudua pale jikoni, akajaa furaha isiyokifani, akaniambia,
“mwanangu, Kimfaacho mtu chake, mwoe Frida mie nipate mkamwana. Usijali maneno ya baba yako.” Maneno ya mama yalinifanya
niduwae maana sikutegemea kama angenambia vile. Nikabaki nimemkodolea macho
mama yangu ambaye alikuwa amejaa furaha tele. Mama akagundua kuwa nilikuwa sina
amani moyoni akanambia “mwanangu, mwoe tu Frida mlete ndani, maana kama baba
yako amesema yule nae ni mtoto wake basi kwa uhakika Frida sio dada yako maana
hata huyo sio baba yako. Kwahiyo, wewe na Frida ni mama tofauti na baba
tofauti, hivyo sio dada yako, wewe mwoe tu mlete ndani!” Nilipigwa na butwaa
kusikia maneno haya ya mama ambayo wala sikuyategemea.
Huku mama
akiendelea na shughuli zake pale jikoni, huku sasa akiwa amejaa furaha,
nilisimama kwa muda kisha nikaondoka, kichwani nikiwa na mafuriko ya mawazo
hata kuhisi nachanganyikiwa. Nikaondoka na kurudi moja kwa moja chumbani
kwangu. Nikajaribu kulala ili kupoteza mawazo ijapo ni bado jioni na chakula
cha jioni bado sijala lakini ikashindikana. Usingizi haukupatikani, muda wote
mawazo yalinivamia na kujikuta namkumbaka mchumba`ngu Frida. Nakumbuka maneno
ya baba yangu, nakumbuka na maneno ya mama yangu, kisha nayalinganisha. Nahisi
ubongo umevurugana, sijui hatima ya maisha yangu na mchumbangu Frida. Nami
naandika kwa mwandiko huu mbaya maana mikono inatetemeka nataka kuomba ushauri
kwako msomaji. Je nifate maonyo ya baba kuto mwoa Frida japo naujeruhi moyo
wangu uliopenda, au je mimwoe Frida nimfurahishe yeye na mama yangu?
Ndugu nami
nimejikalisha chumbani hapa nimenyong`onyea nangoja ushauri wako ili
nikamshirikishe mchumba`ngu Frida.
No comments:
Post a Comment