Pokea
Barua Yangu
BELINDA
Na Mtunzi: Elias Kalistus Mwalongo(KANTON)
Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Ruaha(RUCU)
Simu: 0769313224
TUMA NAMBA YAKO NIKUTUMIE AUDIO YA SIMULIZI HII USIKILIZE BURE
KABISA IKISIMULIWA NA HILALI ALEXANDER TUHUNDWA
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Si
hali yangu ya kawaida, lakini imenipasa kuizoea !!
Belinda,
nimeshazoea sasa. Ni mwaka mmoja sasa umepita. Nimenawa machozi kwa muda mrefu
sana nikikulilia mpenzi wangu, maumivu yakaja kutulia. Asante Mungu!
Belinda,
tukio la leo limenifanya niikumbuke siku ile nilipochota mchanga kwa kiganja changu
na kuutupa ndani ya kaburi lako.
Nimekumbuka
pia ulivyofungwa kama pipi kwenye sanda, ukawekwa kwenye jeneza la saizi yako,
na jeneza likabebwa juu juu mpaka makaburini. Ukazikwa, na watu wakalishindilia
kaburi lako kwa visigino mbele ya macho yangu ishara tosha kwamba hata ungefumbua
macho ili uniage, usingeweza kuniona tena.
Nililia
machozi siku ile kama mtoto mdogo aliyenyang`anywa mdoli wake wa kuchezea. Uso
mzima nilinawa machozi. Kamasi nazo zilichungulia kwenye matundu mawili ya pua
zangu, kana kwamba zilitaka pia kushuhudia mazishi yako mpenzi wangu. Miguu
ilikufa ganzi nisiweze kusimama bila kushikiliwa. Uliniacha sina hali jamani
mpenzi wangu.
Belinda,
tangu umeniacha, leo limenikuta jambo jingine la kusikitisha na kunivunja mtima
wangu, ndilo lililonifanya nichukue kalamu yangu, nikae kwenye kigoda
nikuandikie barua, ujumbe ukufikie, huko uliko. Naomba pokea barua yangu
Belinda.
Nilikupenda
sana Belinda, lakini Mungu alikupenda zaidi. Mipango yote ya kimaisha ambayo
tuliipanga kuifanya pamoja hatujatekeleza hata kiduchu. Tulimwomba Mungu
atujalie watoto wanne waizunguke meza yetu na kuipamba nyumba yetu, Belinda,
umeniacha bila hata mtoto mmoja. Tulipanga tuyajenge maisha yetu, lakini
umeniacha natangatanga peke yangu kwenye dunia hii ya shuruba. Kila tulichokipanga
kimevurugwa na mauti yako. Ukaniacha ninalia machozi, hata nikatamani na mimi
nijifie. Ukizingatia ndo kwanza tulikuwa tunaanza maisha yetu na penzi letu
lilikuwa ndo linachipua. Ugonjwa uliokuvamia ghafla ukaitoa roho yako.
Mama
yangu ndiye aliyebaki kuwa mfariji wangu. Akanifariji nikapoa moyoni, akanifuta
machozi mwanae nami nikatulia tuli. Nafsi ikakubaliana na yote yaliyokuwa
yametokea.
Belinda,
naandika barua hii kwa masikitiko kukutaarifu kuwa mama yangu kipenzi
aliyekupenda, Mungu amemchukua leo alfajiri. Roho yake imemrudia mwenyezi
aliyeiumba na mwili wake umerudishwa mavumbini ulikotoka. Jaribu kupata picha
moyo wangu ulivyopondeka na kuishiwa pozi maskini mimi.
Ulikuwa
kitulizo changu ukaenda zako ghafla bila hata kuniambia “kwaheri”. Mama
aliyebaki kuwa mfariji wangu naye leo ameenda. Achilia mbali baba yangu
aliyenitoka ningali bado mdogo kabisa kwa ajali ya basi asiniachie hata mdogo
wangu.
Kwa
hali hii nani atakuwa mhimili wangu katika kumalizia kipande cha maisha
kilichobaki?. Niko wakati mgumu Belinda, hasa nikikumbuka upendo wako, na
mikakati yetu tuliyoipanga ambayo sasa imepotelea hewani. Nikimkumbuka mama
yangu kipenzi, masalale! Ninahisi kama vile sina la kulifanya tena hapa
duniani, na kama litakuwepo basi halitakuwa la maana tena kwangu. Hata hivyo
natamani ujumbe huu ukufikie huko uliko. Nami naendelea kuganga na maisha hata
pale Mola atakapona inatosha. Naomba uniombee niweze kukabiliana na yote ya
ulimwengu huu shupavu. Namwachia Mola aliye asili wa yote. Naweka kalamu yangu
chini naomba pokea barua yangu Belinda.
KARIBU 0769313224 NIKURUSHIE AUDIO YAKE BURE!

Good story
ReplyDelete