Mtunzi: Elias Kalistus
Mwalongo
Chuo Kikuu Cha Kikatoliki
Ruaha(RUCU)
Simu: 0769313224
____________
Laazizi
wangu wa moyo, natamani nikunong`oneze maneno matamu lakini najikuta niko hoi
tena hoi kabisa, nashindwa nianzeje. Umebarikiwa kati ya waliobarikiwa na
umetunukiwa vyote vigezo.
Hakika
nimekuchagua wewe kati ya waliotunukiwa sifa na vigezo lakini umewazidi mbali
mno. Nikikutazama sura yako wala siwezi kukumaliza leo wala kesho kutwa. Kidevu
kilichochongoka, pua ya saizi halali, shingo kama ya kangaroo na macho ya
yalolegea yenye kukonyeza haki ya nani umeniteka nimekubali tu niwe mateka
wako.
Ole
wangu sasa nione kifua chako chenye mwinuko, mgongo tumbo na kiuno chenye saizi
ile ninayoipenda mimi, mashallah, nahisi labda ni mmakonde fulani kanichongea
vile ninavotaka, kumbe la hasha ni mwenyezi mwenyewe kakuumba kwa ustadi mkubwa
hivyo.
Nyuma
sasa sigeuki na mbele ni siri yangu, lakini mguu wa saizi wenye mvuto, kucha, vidole,
mabega na mikono, nimefumbwa macho sioni kasoro yoyote kwako, amaa hakika
mwenyezi ashukuriwe kwa uumbaji.
Nywele
zako kichwani uziseti vile ninavopenda, halafu masikio utundike na heleni nzuri
zinazongaa uziache tu zinaning`inia kama bangili, walahi sikuachi, naomba
uniteke zaidi, ongeza na walinzi ili nisitoroke.
Ili
nikome kubwabwaja maneno, naomba sogea mpenzi wangu unikumbatie kumbatio la
mahaba, nijilaze kifuani pako huku nikideka kwa deko nawe unidekeze nidekezeke
nisahau shida zote za hapa duniani hata nijisikie niko paradiso najivinjari.
Nikumbate
unipetipeti vyovyote vile maana nishakuwa hoi taabani, akili yangu yote
imehamia kwako sikumbuki kingine chochote. Nikikuangalia usoni muda mwingine
nahisi labda ni malaika fulani kanitembelea kumbe ni wewe laazizi wangu wa moyo
ambaye nimekuchagua mwenyewe. Umesheheni sifa nyingi nami nimekusujudu sina kwa
kwenda kwingine maana kwako ndio nimefika, nimetua mabegi na vilago vyangu.
Tena
sitavuta subira, nitakupeleka ndani uwe mama wa wanangu na mimi ndio baba. Walimwengu
watabaki kutushangaa lakini ukweli utabaki hivyo hivyo. Maneno yao wakiongea
wala usijali maana huwa hawaishiwi ya kusema. Najua tu kuwa ya kwao watayatia
mfuniko na yangu watayachezea mdundiko, wala usiwazingatie.
Nakupenda
wewe tu laazizi wangu, wengine watabaki kuwa wifi zako. Naapa kuwa NITAKUPENDA DAIMA
ili nihakikishe kuwa sikupotezi kwa uzembe.
Naomba
usichoke kunipenda, kamoyo kangu kadogo nimekaegesha kwako kote, naomba
ukatunze kasipate majeraha, nisije nikajifia mwenzio.
Laazizi
wangu wa moyo, nitakupenda daima!
Ahsante sana!
_
