Monday, 20 February 2017

POKEA BARUA YANGU BELINDA- MTUNZI: ELIAS MWALONGO



Pokea Barua Yangu
BELINDA
Na Mtunzi: Elias Kalistus Mwalongo(KANTON)
Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Ruaha(RUCU)
Simu: 0769313224
TUMA NAMBA YAKO NIKUTUMIE AUDIO YA SIMULIZI HII USIKILIZE BURE KABISA IKISIMULIWA NA HILALI ALEXANDER TUHUNDWA
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Si hali yangu ya kawaida, lakini imenipasa kuizoea !!
Belinda, nimeshazoea sasa. Ni mwaka mmoja sasa umepita. Nimenawa machozi kwa muda mrefu sana nikikulilia mpenzi wangu, maumivu yakaja kutulia. Asante Mungu!
Belinda, tukio la leo limenifanya niikumbuke siku ile nilipochota mchanga kwa kiganja changu na kuutupa ndani ya kaburi lako.
Nimekumbuka pia ulivyofungwa kama pipi kwenye sanda, ukawekwa kwenye jeneza la saizi yako, na jeneza likabebwa juu juu mpaka makaburini. Ukazikwa, na watu wakalishindilia kaburi lako kwa visigino mbele ya macho yangu ishara tosha kwamba hata ungefumbua macho ili uniage, usingeweza kuniona tena.
Nililia machozi siku ile kama mtoto mdogo aliyenyang`anywa mdoli wake wa kuchezea. Uso mzima nilinawa machozi. Kamasi nazo zilichungulia kwenye matundu mawili ya pua zangu, kana kwamba zilitaka pia kushuhudia mazishi yako mpenzi wangu. Miguu ilikufa ganzi nisiweze kusimama bila kushikiliwa. Uliniacha sina hali jamani mpenzi wangu.
Belinda, tangu umeniacha, leo limenikuta jambo jingine la kusikitisha na kunivunja mtima wangu, ndilo lililonifanya nichukue kalamu yangu, nikae kwenye kigoda nikuandikie barua, ujumbe ukufikie, huko uliko. Naomba pokea barua yangu Belinda.
Nilikupenda sana Belinda, lakini Mungu alikupenda zaidi. Mipango yote ya kimaisha ambayo tuliipanga kuifanya pamoja hatujatekeleza hata kiduchu. Tulimwomba Mungu atujalie watoto wanne waizunguke meza yetu na kuipamba nyumba yetu, Belinda, umeniacha bila hata mtoto mmoja. Tulipanga tuyajenge maisha yetu, lakini umeniacha natangatanga peke yangu kwenye dunia hii ya shuruba. Kila tulichokipanga kimevurugwa na mauti yako. Ukaniacha ninalia machozi, hata nikatamani na mimi nijifie. Ukizingatia ndo kwanza tulikuwa tunaanza maisha yetu na penzi letu lilikuwa ndo linachipua. Ugonjwa uliokuvamia ghafla ukaitoa roho yako.
Mama yangu ndiye aliyebaki kuwa mfariji wangu. Akanifariji nikapoa moyoni, akanifuta machozi mwanae nami nikatulia tuli. Nafsi ikakubaliana na yote yaliyokuwa yametokea.
Belinda, naandika barua hii kwa masikitiko kukutaarifu kuwa mama yangu kipenzi aliyekupenda, Mungu amemchukua leo alfajiri. Roho yake imemrudia mwenyezi aliyeiumba na mwili wake umerudishwa mavumbini ulikotoka. Jaribu kupata picha moyo wangu ulivyopondeka na kuishiwa pozi maskini mimi.
Ulikuwa kitulizo changu ukaenda zako ghafla bila hata kuniambia “kwaheri”. Mama aliyebaki kuwa mfariji wangu naye leo ameenda. Achilia mbali baba yangu aliyenitoka ningali bado mdogo kabisa kwa ajali ya basi asiniachie hata mdogo wangu.
Kwa hali hii nani atakuwa mhimili wangu katika kumalizia kipande cha maisha kilichobaki?. Niko wakati mgumu Belinda, hasa nikikumbuka upendo wako, na mikakati yetu tuliyoipanga ambayo sasa imepotelea hewani. Nikimkumbuka mama yangu kipenzi, masalale! Ninahisi kama vile sina la kulifanya tena hapa duniani, na kama litakuwepo basi halitakuwa la maana tena kwangu. Hata hivyo natamani ujumbe huu ukufikie huko uliko. Nami naendelea kuganga na maisha hata pale Mola atakapona inatosha. Naomba uniombee niweze kukabiliana na yote ya ulimwengu huu shupavu. Namwachia Mola aliye asili wa yote. Naweka kalamu yangu chini naomba pokea barua yangu Belinda. 
KARIBU 0769313224 NIKURUSHIE AUDIO YAKE BURE!

DADA`NGU MCHUMBA`NGU-Mtunzi: Elias Mwalongo



DADA`NGU
MCHUMBA`NGU
________________________________________________________________













Mtunzi: Elias K. Mwalongo(Kanton)
Ruaha Catholic UNiversity(RUCU)
+255769313224

Umri wangu si haba, ni miaka ya kutosha kuitwa mtu mzima. Hata nikimwambia mtu yeyote kuwa nataka kutafuta jiko hatanishangaa. Hata hivyo sasa nimechanganyikiwa akili, kichwani ni maluweluwe matupu. Najaribu kulala ili nipoteze mawazo lakini usingizi ukiisha mawazo yanarudia yaleyale. Ningekuwa mnywaji mzuri wa pombe, basi ningenunua pombe ya kutosha hata viroba vingi au mvinyo, ili ninywe nilewe hata nikizidiwa hadi kufa wacha nijifie tu.

Ninaikumbuka siku ile ya jumamosi nilipomwendea baba yangu aliyekuwa amekaa sebuleni akiangalia TV na nikamwambia kuwa nimepata mchumba na ninampango wa kumwoa endapo wazazi na ndugu wangeridhia.

Nilimweleza wazi baba yangu kuwa nilipata mchumba aitwaye Frida binti wa mzee Lukengelo. Baba alishituka akanikodolea macho, akanisogelea akaongea kwa kuninong`oneza akasema, “Mwanangu, umri wako unakuruhusu kuoa, umeshakuwa mtu mzima mwanangu, lakini chonde nakuomba usimuoe Frida maana, yule ni dada yako kabisa na baba yenu ni mimi ila naomba mwanangu usimwambie mama yako maana yeye hajui.” Nilimkodolea macho baba, Nilitaka kubishia lakini yeye akaendelea, “mwanangu chonde naomba utafute mwingine lakini usimwoe Frida maana ni dada yako na baba yenu ni mimi ila naomba usimwambie mama yako maana yeye bado haelewi hilo.”

Nilifedheheka na kuhuzunika moyoni kusikia kauli ya baba yangu. Kilichoniumiza zaidi ni ile kauli ya kwamba nitafute mwingine nisimwoe Frida, ukizingatia ni binti pekee ambaye nilimpenda kwa dhati, nilimweka moyoni mwangu. Alinipenda nami nilimpenda kwa dhati, mawazo yangu muda wote yalikuwa ni kwake. Nilimpenda sana Frida, yeye ndiye alikuwa ni shibe ya nafsi yangu na faraja ya moyo wangu. Kumkosa Frida maishani mwangu nilihisi ni sawa na kupoteza kiungo kikubwa mwilini mwangu.

Masaa yalienda kwa kasi, siku zikaja na kupita wiki ya kwanza ikapita. Wiki ya pili nayo ikabisha hodi na kunikuta ningali nafurukuta moyoni kwa hofu ya kumkosa Frida maishani mwangu. Msongo wa mawazo ukanikondesha na kunifanya mnyonge kila muda. Lakini ikafika wakati nikaona uvumilivu umenishinda, nisingeweza kuendelea kuficha siri ambayo baba aliniambia. Nilihisi kabisa mpango wangu wa kufunga ndoa na Frida ulikuwa umegonga mwamba. Basi niliamua liwalo na liwe, wacha niyatoe ya moyoni. Niliamua nimwambie Mama ukweli wote ambao baba alinieleza na kunisihi nisimwambie mama ili lisitokee timbwili lolote pale nyumbani. Kumbuka, msiri wa siri ya moyoni ni mwanasiri mwenyewe. Msiri huiweka siri sirini mwake na pango la siri ni moyo. Moyo wenyewe umeumbwa kisirisiri, hata ukiupasua, kamwe hauwezi kukwambia siri ya msiri. Na siri ni siri kwa upande mmoja tu wa mwanasiri, lakini ikishafahamika na wengine hiyo si siri tena. Na hii siri ya baba haikuwa siri tena maana aliniambia mimi, nami nikashindwa kuihifadhi moyoni nikaamua kumwambia mama yangu ili tu kutua mzigo mkubwa niliokuwa nimeubeba moyoni mwangu.

Ni juzi tu nilimfuata mama jikoni na kumkuta akijishughulisha na mapishi kama kawaida yake. Nikamsalimu kwa heshima aliyonifundisha yeye mwenyewe, kisha nikatulia. Yamkini mama aligundua kuwa nilikuwa na neno la kusema. Akanihamasisha niseme shida yangu, nami nikaanza kusema maana ilikuwa ni shida kweli niliyokuwa nayo. Nikamwambia, “Mama mimi nina neno la kusema” akadakia, “ehee sema mwanangu nakusikiliza” Nikaendelea “ Mama mimi nimepata mchumba…” Kabla sijaendelea mama aliweka bakuli lake chini alilokuwa amelishika, akakaa makini kunisikiliza mimi. Nami nikaamua kuanza upya nikasema, “Mama mimi nimepata mchumba, mchumba wangu anaitwa Frida, binti wa mzee Lukengelo, bila shaka unamfahamu! Mama akasema, “ndio, namfahamu vizuri mzee Lukengelo na familia yake yote na huyo binti uliyemtaja namfahamu. Mwanangu umri wako unakuruhusu, mimi naona umefanya uamuzi mzuri. Jipange mwangu, nitamwambia baba yako na sisi wazazi wako tutajipanga vema” Mimi nilikuwa namwangalia tu usoni anavonifagilia, kisha nikasema, “Lakini mama, nimemwambia baba juu ya suala hili amenikataza kabisa nisimwoe Frida, anasema kuwa Frida ni dada yangu na yeye ndiye baba yetu, ila alinionya nisithubutu kukwambia wewe, nami nimevumilia kwa muda mrefu, nimeshindwa kuendelea kuyaweka moyoni..” Niliongea maneno haya kwa hofu nikiogopa timbwili litakalotokea pale.

Hata hivyo nilimwona mama`ngu akitabasamu kwa furaha. Niliponyamaza kuongea akacheka mamangu kwa furaha, akacheza na kudua pale jikoni, akajaa furaha isiyokifani, akaniambia, “mwanangu, Kimfaacho mtu chake, mwoe Frida mie nipate mkamwana. Usijali maneno ya baba yako.” Maneno ya mama yalinifanya niduwae maana sikutegemea kama angenambia vile. Nikabaki nimemkodolea macho mama yangu ambaye alikuwa amejaa furaha tele. Mama akagundua kuwa nilikuwa sina amani moyoni akanambia “mwanangu, mwoe tu Frida mlete ndani, maana kama baba yako amesema yule nae ni mtoto wake basi kwa uhakika Frida sio dada yako maana hata huyo sio baba yako. Kwahiyo, wewe na Frida ni mama tofauti na baba tofauti, hivyo sio dada yako, wewe mwoe tu mlete ndani!” Nilipigwa na butwaa kusikia maneno haya ya mama ambayo wala sikuyategemea.

Huku mama akiendelea na shughuli zake pale jikoni, huku sasa akiwa amejaa furaha, nilisimama kwa muda kisha nikaondoka, kichwani nikiwa na mafuriko ya mawazo hata kuhisi nachanganyikiwa. Nikaondoka na kurudi moja kwa moja chumbani kwangu. Nikajaribu kulala ili kupoteza mawazo ijapo ni bado jioni na chakula cha jioni bado sijala lakini ikashindikana. Usingizi haukupatikani, muda wote mawazo yalinivamia na kujikuta namkumbaka mchumba`ngu Frida. Nakumbuka maneno ya baba yangu, nakumbuka na maneno ya mama yangu, kisha nayalinganisha. Nahisi ubongo umevurugana, sijui hatima ya maisha yangu na mchumbangu Frida. Nami naandika kwa mwandiko huu mbaya maana mikono inatetemeka nataka kuomba ushauri kwako msomaji. Je nifate maonyo ya baba kuto mwoa Frida japo naujeruhi moyo wangu uliopenda, au je mimwoe Frida nimfurahishe yeye na mama yangu?

Ndugu nami nimejikalisha chumbani hapa nimenyong`onyea nangoja ushauri wako ili nikamshirikishe mchumba`ngu Frida.



NITAKUPENDA DAIMA

Mtunzi: Elias Kalistus Mwalongo Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Ruaha(RUCU) Simu: 0769313224 ____________ Laazizi wangu wa moyo, nat...