Thursday, 26 January 2017

MAKALA ZA KANTONI



MAKALA ZA KANTONI ZILIZOTOLEWA KATIKA GAZETI LA MWENGE KWA MATOLEO TOFAUTI TOFAUTI.

KALIA KIGODA MWANAKWETU, BURUDIKA NA TUNGO MWANANA TOKA KWA MWANDISHI WAKO WA SIKU NYINGI

ELIAS MWALONGO

(KANTON)




“WATOTO WA SIKU HIZI, HOVYO KABISA!!”

Kuna kauli nyingi zinazoweza kusikika mitaani zinazowashutumu vijana wa karne hii.Kuna kauli kama za “watoto wa siku hizi hawasikii” au “watoto wa .com hovyo kabisa”. Hiyo kauli ya `.com` ni ya kisasa kidogo ukiilinganisha na hiyo nyingine ya `watoto wa siku hizi`.
Nakumbuka kauli hiyo nilikuwa naisikia tangu nikiwa mdogo(mtoto) kwenye miaka ya 90,91.Nilikuwa nawasikia watu wazima wa nyakati hizo wakilalamika kuhusiana na watoto wa nyakati hizo(sisi) yaani tulikuwa hatusikii.Malalamiko hayo yalikuwa yanakwenda hata kwa vijana wa wakati huo.Walikuwa wakilalamikiwa na kuwa tabia zilizokuwa zinahesabiwa kuwa mbaya siku hizo.Nakumbuka moja kati ya tabia hizo iliyokuwa inalalamikiwa kwa upande wa wasichana wa nyakati hizo ilikuwa ni uvaaji wa suruali.Watu wengi wa sasa wanaweza kushangaa kama uvaaji wa suruali ni tatizo.Lakini ndivyo ilivyokuwa japo kwa sasa tunachukulia ni vazi la kawaida kwa wasichana,hatushangai.
Binti aliyekuwa anavaa suruali alionekana kama Malaya sana siku hizo na alionekana kama aliyeshindikana, siku hizi ni kawaida,Lakini tatizo la watoto na vijana kulalamikiwa limekuwa likiongezeka na kuwa kubwa zaidi kila kukicha na kweli tabia za ajabu za watoto na vijana zimekuwa zikistaajabisha sana.
Siku hizi si ajabu ukasikia kesi za vitoto vya miaka 6-10 vikicheza kamali,vikiiba,vikijihusisha na madawa ya kulevya pia hata kujihusisha katika mapenzi.Vitoto vya kiume unaweza kukuta vikivaa “kata K,modo” na mavazi mengine yasiyo ya heshima.Wasichana nao wana yao mengi tu.Vibinti vidogo tu unaweza kuvikuta vinavaa vimini mitaani bila aibu,vingine vinajiuza na mbaya zaidi havitaki kusoma shule.Na matukio mengine mengi ambayo kila mmoja anaweza kuyashuhudia katika jamii yake.
Unaweza kujiuliza, hawa watoto na vijana wanazitoa wapi hizi tabia za ovyoovyo! Wengine wanasema “utandawazi” Wengine wanasema eti ni “nyakati za mwisho” ilimradi kila mtu amesema lake.Lakini je ni kipi chanzo cha tabia hizi mbaya?Je watoto wenyewe wanajitafutia?Je kuna mahali wanajifunza? Watoto hawa wameonekana kanakwamba wao wenyewe wamekuwa wakijibadilisha toka uzuri kwenda ubaya.Jambo ambalo wao hubebeshwa lawama kwa tabia hizo na kuonekana kero katika jamii zao.Mimi sikubaliani na majibu hayo hata kidogo!
Kuna nadharia moja inasema “kuku hawezi kutaga yai bovu,ila uatamiaji wake ndio unaoamua kuwa yai liwe bovu au liwe bora.Kama kutakuwa na umakini katika uatamiaji basi hakuna hata yai moja litakalokuwa bovu au kuharibika.Nikija kwenye suala la tabia za watoto na vijana,hakuna tofauti.Hakuna ambaye hafahamu kuwa watoto hawajileti,au kujiamulia kuzaliwa hapa duniani. Sio yeye atakayeamua azaliwe au laa.Hiyo ni kadiri ya kanuni ya maumbile na haina ubishi.Na mtoto akishazaliwa,binadamu wa kwanza kukutana naye ni wazazi wake hasa mama.Lakini pia utafiti wa kibaolojia unaonyesha kuwa mtoto anapokuwa tumboni mwa mama yake anaweza kujifunza tabia za mama yake hasa kwa kusikiliza anavyoongea.Hivyo mama akiwa na matusi na mtoto hujifunza hivyohivyo.Mama akiwa mlevi wakati wa ujauzito na mtoto kuja kuwa mlevi ni asilimia tisini.Pia baada ya kuzaliwa, mtoto hukua mikononi mwa wazazi wake hasa mama, kwa kuwa wakati mwingi anakuwa nae.Hivyo basi, kama wazazi watakuwa na tabia mbaya mbaya hatutashangaa na watoto wao wakiwa hivyohivyo.Lakini sikuhizi katika familia nyingi watoto hulelewa na mahousegirl.Je, hii si hatari kwa malezi ya mtoto?Mtoto ataiga tabia za housegirl badala ya kuiga tabia za wazazi wake.Kama housegirl ni msagaji, Malaya,shoga,mwizi n.k.Je, mtoto ataiga nini?Ndipo wataibuka watoto wenye tabia za ovyo ambazo hata wazazi wanazishangaa.Wataendelea kuibua lawama nyingi kwa watoto na vijana hawakumbuki kuwa “mtoto umleavyo ndivyo akuavyo”.Hivyo kwa mtazamo wangu naona mtu wa kwanza kulaumiwa kwa tabia mbaya za watoto na vijana na mmomonyoko wa maadili kiujumla Mzazi/mlezi ndio awe wa kwanza kunyoshewa kidole.Kwani katika malezi ya mtoto kuna walimu watatu,wa kwanza ni mzazi,wa pili ni mwalimu wake shuleni,na watatu ni ulimwengu ambao utamfundisha yule aliyekosa malezi ya walimu wawili waliotangulia.Kwahiyo kauli za “vijana wa sikuhizi hovyo kabisa”zisiwalenge vijana au watoto moja kwa moja,bali tuangalie hawa vijana wanalelewaje katika jamii zao!!

                       

Na; Elias K. Mwalongo(KANTON)
Ruaha Catholic University(RUCU)
+255769313224





















“KANISA KATOLIKI LIMETUKANWA SANA”


Ndugu msomaji, usije ukanikuda roba, haya wala si maneno yangu.Ni nukuu ya maneno ya mwanzo kabisa ya hotuba ya Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki la Mbeya,Tanzania aliyoongea wakati akitoa ufafanuzi wa tamko la jukwaa la wakristo kuhusu suala la kuchoka kutukanwa kuchokozwa na kuonewa kwa Kanisa Katoliki.Askofu Chengula alisema sio dhana ya kulipiza kisasi bali ni kuwa watu wa sala, kitubio na ikiwezekana kukaa na kuzungumza na wanaofanya chuki na Kanisa katoliki na kufanya uharibifu wa mali za watu na serikali.
            Askofu Chengula alitoa ufafanuzi huo katika semina ya Makatekista na walimu wa dini iliyofanyika katika ukumbi wa vijana Jijini Mbeya tarehe 2-2-2013, ambao walitaka kujua ukimya huo utadumu mpaka lini hali wanachokozwa,wanatishiwa maisha na na vitu kuharibiwa.Alisema kuwa licha ya kanisa kutukanwa,kuchokozwa na kuharibiwa mali na hata kufikia hatua ya kuwapiga risasi baadhi ya viongozi wa kanisa,Kanisa katoliki halitajibu zaidi ya kuendelea kusali Rozari Takatifu, kufanya kitubio na kuendelea kufunga ili kushinda majaribu yasiyompendeza Mwenyezi Mungu.
            “Kanisa Katoliki limetukanwa sana,limefanyiwa uchokozi na uharibifu mkubwa na sasa wameanza kutupiga na bunduki,huku vikitolewa vitisho vya kuuawa mapadre na maaskofu waziwazi.Lakini tunaposema Kanisa limechoka kutukanwa msibebe bunduki, bali muwe watu wa sala na kuwaombea wanaofanya hayo ili watubu na wamrudie Mwenyezi Mungu”.Aliongeza “Muwe watu wa sala,mapatano na wakakamavu.tusali Rozari katika nyumba zetu tufanye kitubio na tuwe watu wa kufunga na kumshinda shetani, hiyo ndiyo silaha pekee na ikibidi kutokana na kuchoka huku tuwe tayari kuzungumza na hao wanaotuchokoza.”
            Aidha, alitoa ushauri kwa serikali na mamlaka husika kutoruhusu kujenga nyumba za starehe karibu na shule au vyuo kwani ndio chanzo kikubwa cha ongezeko la vitendo vya kikatili vya utoaji mimba n watoto wanaookotwa katika madampo ya taka katika vyuo na mashule.Alisema haiwezekani shule na starehe.Hivyo kujenga majumba ya starehe ni kumjengea mwanafunzi mazingira magumu ya ushawishi na ndio matokeo ya kushindwa kuendelea na masomo vizuri.
            Hata hivyo aliwaagiza mapadre, watawa wa kike na wakiume, makatekista na walimu wa dini kuongeza jitihada za dhati kutembelea mara kwa mara wanafunzi na wanachuo kuwapatia ushauri licha ya kuendelea kutoa mafundisho ya dini ili waweze kufuata maadili mema.Katika semina hiyo mambo mbalimbali yalizungumzwa kuhusu muhtasari wa mafundisho ya dini kuanzia shule za awali hadi vyuo vikuu,ambapo Katibu mtendaji wa idara ya katekesi kutoka Baraza la Maaskofu Tanzania,Pd. Raphael Madinda alitoa mada kuhusu umhimu wa wizara ya Elimu na mafunzo ya ufundi kuridhia kuingizwa katika mtaala wa Elimu nchini. Pd. Madinda alisema mmomonyoko wa maadili na kuibuka kwa vurugu, migomo na migogoro mbalimbali hata kusababisha maandamano mashuleni,chanzo kikubwa ni ukosefu wa mafundisho ya dini ambayo humjenga mwanafunzi kumuogopa Mungu na kuishi kwa kufuata,sheria za nchi, maadili na utu wema.
            Alitoa wito kwa waamini wa kanisa Katoliki kujitokeza kwa wingi kutoa mafundisho ya dini kwa wanafunzi kuanzia ngazi za awali,  msingi, sekondari, vyuo na vyuo vikuu  ili jamii iweze kurejea katika maisha ya upendo, amani, utulivu, upatanisho, haki na kuvumiliana,mambo ambayo yanaendelea kuporomoka kwa kasi ya ajabu nchini Tanzania.
            Katika semina hiyo,Pd. Innocent Sanga amesema changamoto kubwa wanayokabiliana ni ukata katika kuwawezesha walimu na makatekista kufundisha katika shule mbalimbali kwani jiografia ya maeneo ya mkoa wa Mbeya ni milima na mabonde na shule hujengwa umbali mrefu unaohitaji vyombo vya usafiri na fedha za kujikimu jambo ambalo wanaendelea kulitafutia ufumbuzi wakati wakiendelea kujitoa.
     Hata hivyo Askofu Chengula wakati akigawa vitabu vya muhtasari wa mafundisho ya dini mashuleni amewapongeza mapadri kwa kuendelea kutoa mafundisho ya dini kwani hilo ndilo jukumu kubwa la kanisa kufundisha katekismu, Neno la Mungu maisha ya kisakramenti na huduma nyingine za kiroho ya kimwili.



Na; Elias K. Mwalongo(KANTON)
Ruaha Catholic University(RUCU)
+255769313224

















KEKI  ISIYOOZA


Huenda mimi na wewe tumekuwa tukijitahidi mara kwa mara kutengeneza keki bora lakini hazidumu.Tunatengeneza kwa ufasaha tukidhani zitadumu lakini zinaoza ovyoovyo.Fuatilia sasa hatua hizi za kutengeneza KEKI ISIYOOZA;
Chukua kiasi kikubwa cha uchangamfu.Angalia kwanza kwa makini kisiwe kikubwa sana.Changanya na bakuli moja la upendo katika chombo kiitwacho Biblia.Ongeza walau vikombe vikubwa viwili vya ukarimu.Weka kijiko kimoja kikubwa cha tabasamu.Koroga mchanganyo wako kwa makini,koroga kwa nguvu kwa dakika kumi ili viungo hivyo vijichanganye vizuri.Kisha ongeza kikombe kidogo cha nia,koroga vyote pamoja kwa dakika mbili.Kisha chukua chujio ya uwazi,chuja mchanganyo wako ili kuondoa takataka za ubinafsi,choyo,wivu,dharau,umbea,uvivu,chuki,kiburi,unafiki na takataka nyingine ambazo huenda ziliingia kwa bahati mbaya wakati unaandaa viungo.Ukiisha chuja takataka hizo kung`utia mbali huko na uzisahau zisijechafua keki yako baadae.Kisha acha mchanganyo wako kwa dakika kumi au zaidi ili utulie kabisa.Kisha oka keki yako kwenye jiko la heshima,ili iive taratiiiibu kwa joto la sala.Baada ya nusu saa fungua jiko lako,chukua kitambaa cha imani na utumie kuipua keki yako.Ikiwa bado ya moto kabla haijapozwa na baridi ya unafiki,iweke kwenye chombo chenye matundumatundu ili harufu nzuuuri ya upendo iweze kupenya na kuenea katika chumba.
Kiweke chombo hicho sehemu ya uwazi ili harufu nzuri ya keki iweze kuenea kwa watu wengi zaidi nao wafurahi kwa tabasamu la umoja.
Japo najua watu watakunyoshea kidole,watakusodoa na kukuvunja moyo utakapokuwa unafurukuta kutafuta viungo vya keki yako,wala usife moyo.Wengine watakusimanga,watakubinulia midomo,wengine watatamani kukutemea mate,usijali! walimwengu ndivyo walivyo.Yatakapokukuta haya nakusihi ufunge mshipi ujizatiti upige hatua maadamu umedhamiria na unajua unachofanya.Keki yako ikisha iva ndo  kabisa watajaa kijicho,watakukunjia ndita bila kosa,rafiki zako watageuka adui zako ila huenda usigundue maana wakijaa unafiki wanakuwa sivyo walivyo.Usoni watatabasamu huku mioyo ikiwa imekunja ngumi tayari kukuvizia na kukubonda uzime kama kibatali.
Ukishafanikiwa watajaa jeuri,wengine hawatapenda hata kukusikia ukiwaambia “shikamoo,mambo,vipi,poa,shwari,niaje” hata mengine yenye maana sawa na haya.
Siku zote ukifanikiwa si wote watakupigia makofi kwa lengo la kukupongeza.Wengi watakaokununia ni wale wa karibu yako.Nakusihi ukazane kutengeneza keki isiyooza maana inampendeza hata yeye aliyekuumba.Maneno na masimango ya watu yasivurugie mipango yako na kukurudisha nyuma kirahisi.Masimango na wivu wao vikusaidie kupiga hatua mbele zaidi ili uwaache watembee vichwa chini kwa soni.Maana maisha ni mchezo wa Sandakalawe mwenye kupata anapata.Talanta zetu ni tofauti,ukikosa moja haimaanishi huna zote,uliyopewa wewe jivunie maana mwenzako amekosa.Itumie talanta hiyo kwa makini na uaminifu ili ilete manufaa kwa wote.                                              


Na; Elias K. Mwalongo(KANTON)
Ruaha Catholic University(RUCU)
+255769313224



 


SOTE TUNASAFIRI


Mpendwa msomaji, yamkini mimi na wewe ni mashuhuda wa majanga yanayotukumba hasa katika dunia ya leo. Leo dunia inatutunishia misuli,inatutishia na kutugaragaza ovyoovyo.Tunazika ndugu zetu tele wanaotutangulia mbele ya haki kutokana na vita,maangamizi,njaa,magonjwa na wengine wanajipiga kitanzi kutokana na kukata tamaa ya kuendelea kuishi.Leo vyombo vyetu vya habari vinatujuza idadi ya maiti mahututi,mateka,wakimbizi,wala rushwa,biashara feki,divisheni ziro,madawa ya kulevya,ufisadi,migomo,ongezeko la wajane na yatima na matimbwili kadha wa kadha yanayotupiga danadana na kutufanya tutoe machozi kila uchwao.Haki, amani na usawa walizotuachia waasisi wetu vimegeuka karaha tupu.Hata hivyo tushukuru Mungu mimi na wewe bado tunavuta pumzi kwenye dunia hii ambayo wengi wetu wameikatia tama.Lililopo mbele yetu sasa ni kufunga mshipi, kunusuru roho zetu na za wenzetu ili maisha yaendelee.
            Mara nyingi ugumu wa maisha tunaoulalamikia ni wa kujitakia wenyewe.Sikuhizi watu wengi tunafikiria maisha ni leo tu,tunasahau kuwa kesho nayo siku.Na ili kuiandaa hiyo kesho tukisema tuanze kuwakalisha kwenye semina babu zetu na bibi zetu, tutakuwa tunapiga kwenzi kinyago.
Hivyo basi ni jambo la busara tuanze kuwaandaa vizuri vijana na watoto,tukiwajenga vema katika misingi ya malezi bora kiutu,kielimu na kinidhamu.Mazingira pekee ambayo hili linaweza kufanyika ni katika mashule.Harakati hizo za kujinusuru na ugumu wa maisha zianzie shule ya msingi,sekondari mpaka vyuo vikuu.Vijana wafundishwe mambo ambayo yatawafanya wawe na mchango katika jamii zao na nchi kiujumla na sio kukumbatia bahasha nyingi zilizojaa vyeti ambavyo haviwasaidii zaidi ya kuwapa maujiko tu.Katika makongamano mbalimbali ndio nafasi muafaka wa kujenga kizazi kipya kitakachopiga teke rushwa na ufisadi.
Kunaongezeko kubwa la vijana mitaani wanaolalamika kuwa hawajapata ajira serikalini.Lakini wengi wao ukiwaona ni kweli wanastahili kutoajiliwa.Na kwa namna hiyo basi kelele za kulilia ajira hazitakoma na ugumu wa maisha utaendelea kushika kasi.Nakusihi kijana wa leo utegemee sana kipaji chako na ujasiliamali, kuliko kuililia serikali kama vile inakuangalia wewe tu.Tunamifano dhahiri ya watu walio kuwa na maisha duni katika jamii zetu lakini leo maisha yamewanyokea hata tunawaona si wenzetu tena.Je,hawa wametokeje kama sio kujituma tuu!Kwakuwa inawezekana kabisa kijana mwenye nguvu na akili timamu kujitegemea,basi nawasihi vijana fungeni mikanda,maisha lazima yaendelee!!Mida ya kuomba imekwisha na tabia ya kuombaomba au kudokoa vya watu ife.Kwa kuwa unayemwomba na yeye anashida zake ndio maana anapigania kupata na unayemdokolea hujui amepataje,ukikamatwa utabondwa mawe au utachomwa moto uwe majivu kijingakijinga tu.Ili haya yasiendelee kutukumba vijana wa leo,basi vijana,KUFA NA KUPONA, MAISHA LAZIMA YAENDELEE!!




Na; Elias K. Mwalongo(KANTON)
Ruaha Catholic University(RUCU)
+255769313224























IMANI ZA WAZAZI JUU YAWATOTO WAO.


            “…..nusu ya kwanza ya misha yetu huharibiwa na wazazi na nusu inayobaki huharibiwa na watoto wetu”. Ni kauli  iliyosemwa na mshauri wa masuala ya ndoa na malezi Bi. Jenifa James kauli hii ni ngumu ikiwa hukuwahi kufikiria juu ya malezi ya watoto .
        wazazi na walezi popote duniani wanatambua hakuna jukumu zito kama la kulea watoto.Ni kazi ngumu ambayo haina likizo.Ndiyo si ajabu kuona watoto wengi wakitelekezwa lakini haya yote haya wazuii wazazi makini kulea watoto kuwapatia watoto wao huduma ya elimu, afya,mavazi, malezi na mengineyo mrngi ikiwa ni pamoja na usalama wa maisha yao.
            Kumekuwa na imani kadha wa kadha za wazazi katika tamaduni mbalimbali juu ya watoto wao.Wazazi au walezi wanapolea watoto wao hupitia vipindi tofauti ambavyo hubadili mitazamo yao.
           
I.Watoto huimarisha ndoa.
Wanandoa wachanga hutamani sana kupata watoto wakiamini kuwa ndoa itakuwa imara zaidi.Naamu ndivyo ilivyo,watoto huwa kiungo kizuri cha ndoa kinachokazia muungano wa wazazi kwani kila mmoja hujiona anamchango kwa mwenzake.
LAKINI,Wazazi wanapaswa wawe na busara,maana katika  ndoa nyingi watoto wamegeuka mtihani na kutishia kuvunjika kwa mahusiano(ndoa)
           
II.Wazazi wa leo si bora kama wa jana.
Japo si wote lakini sehemu kubwa ya malezi ya watoto imekuwa inaleta utata na kusuasua kana kwamba wazazi wamejiondoa katika jukumu hilo.Katika hali hiyo jamii pia imechangia sana, maana inataka wazazi walee watoto wao katika democrasia,kujali kila hisia ya mtoto,kuwaacha watoto waamue wapendavyo,kinyume cha hapo mkono wa sheria utaingilia kati.Hali hii hupelekea watoto kuyumba kimaadili wakijiona wako sahihi kwakuwa wako huru.
           
III.Ndoa isiyyo na watoto haina furaha.
Wanandoa wengi hawana watoto,wanaishi kwa amani uvumilivu na kupendana.Furaha inaweza kupatikana kutokana na maamuzi ya kuamua kufunga kizazi,kuchelewa kupata watoto n.k.
LAKINI;Ukweli unasimama tena,wanandoa wasio na watoto hawana furaha ya kweli.

IV.Mtoto mmoja hatoshi.
Watafiti Olson naDefrain wanasema;”…mtoto mmoja hana gharama katka kumtunza na habani sana uhuru wa wazazi kuishi wapendavyo na ni rahisi kuishi kwa starehe”
LAKINI;Ikumbukwe kuwa ni rahisi mtoto mmoja kudeka,kunyimwa uhuru wa kucheza na wenzake kwa hofu ya kudhuriwa,na ndio maana wazazi wengi wa Afrika wa zamani na wale wasiobadirika kirahisi walihimiza uzo wa watoto wengi ili kuepuka presha za kupanda na kushuka.

V.Malezi huwa rahisi kadiri mtoto akuavyo.
Hii ni imani iliyoenea lakini inapotosha ukweli halisi.Kadiri watoto wakuavyo ndio malezi huwa magumu zaidi.Tukiacha kipindi cha balehe,kipindi cha kuelekeza watoto wakuaji,wanaokutana na maarifa ya kila uchao katika ulimwengu wa dijitale ni jukumu kubwa zaidi.
           
VI.Malezi huishia watoto wanapoanza kujitegemea na kuondoka nyumbani.
Hii nayo ni imani inayopotosha uhalisia.Wazazi wenye watoto wakubwa ni shahidi wa jambo hili.Hupumzika warudipo enzi za ujana wao kabla ya watoto.LAKINI;
Maranyingi wazazi hao hujikuta wakiishi na watoto,wanapopewa talaka,wanapokosa ajira,wanapofukuzwa kazini,nyakati za migogoro na nyakati za kuachiwa jukumu jipya la kulea watoto wa watoto wao yaani wajukuu wao.

Hitimisho.
Ni vema wazazi wa jana,leo na kesho wakumbuke kuwa kazi ya malezi inashukurani kidogo,ni jukumu la uhai wote na halina malipo.Hivyo wazazi wakumbuke kuwa “mbwa hajifunzi kuwinda uzeeni” na “samaki mkunje angali mbichi” jinsi watakavyo wanyoosha watoto wao wangali wadogo ndivyo watakavyofarijika zaidi baadae na kuyaona matunda mema ya watoto wao.
WATOTO NI ZAWADI KWENU, SIMAMENI IMARA KATIKA MALEZI ILI BAADAE WAWE FARAJA KWENU!

Na; Elias K. Mwalongo(KANTON)
Ruaha Catholic University(RUCU)
+255769313224

No comments:

Post a Comment

NITAKUPENDA DAIMA

Mtunzi: Elias Kalistus Mwalongo Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Ruaha(RUCU) Simu: 0769313224 ____________ Laazizi wangu wa moyo, nat...