Friday, 20 January 2017

SIMULIZI: NITAKUFA NA MTU!



OLE WAKO MIMI NIFUKUZWE SHULE

NITAKUFA NA MTU

Na: Elias K. Mwalongo(Kanton)

MAOMBOLEZO YA MTOTO MCHANGA TOKA KABURINI KUMLILIA MUNGU!

I
likuwa siku ya  Jumamosi fulani (Weekend) Anton (ambaye baadaye atakuwa baba yangu) na Anna (ambaye baadaye atakuwa mama yangu), baada ya mlo wa mchana walitoka hapo shuleni X na kuongozana katika matembezi yao. Baadaye walifika BANDA-BEACH. Baba Anton alitaka kumsadikisha Anna kuwa yeye ni Kizito, alimnywesha ile mbaya akalewa hadi chakaraa. Walipoamua kurudi shuleni, giza nene lilikuwa limeshaingia. Wote wawili wamelewa hoi kabisa. Sasa hata tamaa zao za mwili ziliwatawala.
      Baba Anton  akaanza kumshikashika Mama yangu Anna na kumbeba, akisema, “Anna,amaa kweli,mtoto wewe unanikosha kweli,nami nimekusujudu ile mbaya. Onyesha basi kuwa nawe unanipenda kwelikweli. Tazama hapa tupo kichakani, tena ni giza hakuna anayetuona”. `Naye Mama yangu Anna yupo hoi kabisa, hana hili wala lile anakuballi yote tu. Hivi ndivyo Baba yangu Anton  na Mama yangu Anna walivyojuana usiku ule wa giza kwa kufichama kwa watu pale kichakani, ati watu hawatuoni. Maskini Baba yangu Anton na mama yangu Anna, pale kichakani walidhani wamejificha mbele ya watu, kumbe wasijue kuwa Mungu alikuwa mbele ya macho yao, maskini wazazi wangu!.
HAWATUONI `Ee; Mungu niende umbali gani Ili nijifiche mbali nawe? Nikisema nipande juu sana  Mbinguni, huko ndiko uliko Ee Mungu. Nikitwaa mbawa za asubuhi ili nifike Mashariki ya mbali, hata huko mkono wako wenye nguvu utanifikia Ee Bwana. Nikijificha katika giza nene,giza nalo ni sawa na mchana mbele yako Ee Bwana. Basi niende wapi au nijifiche wapi ambapo Mungu hayupo ili niweze kutenda uovu huo? Sote hapa duniani ni kama sisimizi tu mkononi mwako Ee Bwana, kwa sababu Enzi yako ni kuu mno;Ni nani aliyepima maji yote ya Ulimwengu kwa konzi ya mkono wake?(Isa;40:12ff)Na kuzikadiria Mbingu kwa shubiri,na kuyashika mavumbi ya dunia katika pishi,na kupima milima na vilima kwa mzanii?Ni nani aliye mfundisha Mungu njia ya hukumu,na kumfunza maarifa na kumwonyesha njia ya fahamu? Tazama mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani;  tazama,si kitu mbele zake, huhesabiwa kwake kuwa duni na si kitu ni ubatili. Basi mtamlinganisha Mungu na nani? Au mtamfananisha na mfano wa namna gani? Je, hamkujua toka mwanzo kuwa yeye ndiye azitandazaye Mbingu kama pazia, na kuzikunjua kama hema ya kukaliwa,ndiye awatanguliaye wakuu na kuwabadilisha hao waamuzi wa dunia!.`

ΓΌ MATOKEO YA ULEVI ULE

Siku ile Baba yangu Anton na Mama yangu Anna walivunja sheria ya shule kwa kutofika shuleni kwa rollcall. Siku ile walipoteza hela katika ulevi na uzinifu, siku ile waliharibu afya zao za roho na za mwili, siku ile walipoteza heshima yao kwao wenyewe na kwa watu waliowaona, siku ile walijitenga na Mungu kwa ulevi na uzinzi, siku ile walirudi shuleni maskini na maskini zaidi kiroho, siku ile walimleta mtoto (mimi) duniani watakayemwua baadaye. Siku ile walibaini kuwa Elimu walioipata haikuwasaidia kitu, Imani/dini yao bado haikuwakomboa, wala mazingira hayakuwakomboa na hawakuwa na nidhamu. Pia siku ile nililetwa duniani na wazazi kutokana na ulevi wao tu.

JANUARI 5; Uzima wangu umeanza leo. Ndio siku ile waliyokutana wazazi wangu pale kichakani kwa sababu ya ulevi wao. Lakini wao mpaka sasa hawajagundua mwanzo wa kuishi kwangu. Ningali mdogo sana hivi wala sionekani kwa macho matupu ila kwa darubini kali ninaonekana kama kichwa cha sindano. Lakini hata hivyo tayari mimi ni mtu  kamili niliye nafsi yangu kabisa. Mambo yangu yote yamejisuka kabisa. Maumbile yangu na tabia yangu tayari inaeleweka, Mfano; Macho yangu yanafanana na ya mama yangu, na nywele zangu zinafanana na zile za Baba yangu, za mviringo na nyeusi.Tazama tayari imeshadhihirika kuwa nitakuwa mvulana. Na Mungu tayari anataka niwe Padre wa kuzipeleka Roho za watu tele kwake.

JANUARI 19; Sasa mishipa yangu ingawa ni midogo sana, imeanza kukua na chembe za damu yangu zinaendelea kutengenezwa haraka sana. Bila shaka sasa hivi hakuna hata kiungo kimoja kilichokamilika. Kumbe, bado nategemea damu ya mama yangu inayoniwezesha kuendelea kuishi hadi sasa, kama chakula changu, bado nitamtegemea sana yeye hata baada ya kuzaliwa kwangu, maana ndicho pekee chakula changu bora.

JANUARI 23; Sasa hata midomo yangu imeshakua, kutosha kuweza kuifungua. Baada ya miezi 12 tu au hata pungufu, nitakuwa nikitumia midomo hii kuwasalimu wazazi wangu kwa tabasamu na kwa gugumio la furaha tele na neno la kwanza kulitamka litakuwa “MAMA” Je, Mama yangu hatafurahi kusikia sauti hii nyororo ya mtoto wake!?

JANUARI 25; Hata moyo wangu sasa  umeanza kupigapiga. Na utaendelea kudundadunda daima hadi mwisho wa maisha yangu. Je! Unaonaje? Hii si ajabu na ya kupendeza kwa wote wenye mapenzi mema?

FEBRUARI 2; Kumbe sasa hata mikono na miguu yangu imeanza kukua. Ndiyo, nafahamu kuwa bado itanichukua muda mrefu ili kuitumia vema baada ya kuzaliwa kwangu. Haidhuru, nitavumilia bado!

FEBRUARI 12; Kumbe sasa hata vidole vyangu vya mikononi vimeanza kukua. Hii ni ajabu sana, kwa sababu, mikono yangu hii itashikana na watu wote nitakaokutana nao. Na mikono hii itaweza kujifanyia marafiki tele, kwa kusalimiana na kushikana nao. Kujifanyia kazi yangu mwenyewe, kama vile kusali Misa Takatifu, kugawa Komunyo Takatifu, kuungamisha, kubatiza watu, kupaka watu mafuta matakatifu n.k.

FEBRUARI 20; Tangu siku ile Mama yangu amegundua kuwa hakwenda hedhi/mwezi, halafu alijisikia kutapika, ukinaifu, kukosa hamu ya chakula, maumivu na uvimbe kidogo wa matiti yake, leo aliamua kwenda kumwona mganga.Naye mganga maskini wa unyofu wake wote, alimhakikishia kuwa asiwe na shaka yoyote,mimi nilikuwa nimetungika mimba na ni mzima kabisa na nipo njiani mwa kuzaliwa.
          `Oh!Oh!!!` Alitamka Mama yangu. Hizi zilikuwa ni habari mbaya kabisa, zilizomtoa roho mama yangu hata kuchanganyikiwa akili na kukonda rohoni. Alipiga masumbwi (ngumi) tumbo lake ili kuniua kama ingewezekana. Alilia machozi kumtiririka machoni na kujenga chuki sana juu yangu na hata juu ya Baba yangu Anton, kwa sababu nimetungika mimba. Hakuamini maneno ya mganga.
Siku ileile, alienda mbio na kwa  hasira sana kwa baba yangu Anton. Salamu ya kwanza aliyoweza kutoa kwa Baba yangu Anton aliyekuwa chumbani kwake, Bweni la wavulana alisema, “Ninamimba yako Anton, Ole wako nikifukuzwa shule”, Baba yangu Anton nilimwona kama aliyechanganyikiwa akili. Alikunja ndita,  macho yalimwiva na kamasi kumtoka ovyoovyo tu, aliondoka mle chumbani akatawanyika zake porini.

FEBRURI 25; Mimi bila kujua hili   wala lile analowaza Mama yangu. Nilitamani watu wawambie wazazi wangu kuwa Mimi ni mvulana. Hivi tangu sasa wangeweza kuanza kufikiria jina kwaajili yangu. Lakini kadiri siku zilivyoendelea mbele nilonja sipati tena upendo wa mama yangu bali chuki na ubaridi. Nilianza kuonja upweke kabisa. Laiti ningalijua yanayoningojea masikini!!!!.

FEBRUARI 28; Sasa viungo vyangu vyote vimekuwa vikumbwa, vimekamilika tayari, vyororo na vinapendeza hata kuvitazama.

MACHI 10; Nywele zangu tayari ni nyeusi sana, na macho yangu ya kikahawia (brown) yameanza kukua. Je!Mama yangu sasa hata furahi kuona macho yangu yanafanana sana na yake? Na nywele zangu za mviringo zinafanana na za baba yangu? Hata mimi mara baada ya kupata fahamu nimejiandaa kutoa tabasamu kubwa sana pale nikapoziona mara ya kwanza sura za wazazi wangu wapenzi.

MACHI 13; Bado kitambo kidogo sana sasa hivi karibu nitaweza kutazama mimi mwenyewe kwa macho yangu. Bado kuna ubapa mwembamba tu unaonizuia nisifungue macho yangu. Natamani daima na kungojea kwa hamu kubwa macho yangu yataona nini na rangi ya vitu vya dunia hii. Lakini kuliko yote, furaha yangu kubwa sana itakuwa hasa kuwaona wazazi wangu. Kwanini sasa inachelewa kufika upesi?
Mama yangu  wee! kumbe kuna bado miezi mingine sita ya kungoja!! Lakini haidhuru nitavumilia bado vilevile!

MACHI 24; Tazama, hata moyo wangu sasa umekamilika. Tena hauna dosari yoyote. Ahsante  Mungu, moyo wangu ni salama salimini. Sasa nafurahi nitakuwa mtu mwenye afya nzuri. Nitayafurahia maisha yangu kwa kujifanyia kazi zangu mwenyewe.

MACHI 28; AAAHHH!!! Mungu wangu weee! Leo Mama yangu Anna, ameniua maskini mimi,  jamani.
Tangu siku ile alipomwendea yule mganga naye alipomwambia kuwa nilikuwa nimetungika mimba, amekuwa akikutana na Baba yangu mara nyingi sana, nao kila mara walijadiliana mengi ya ugomvi, matusi, chuki na kero nyingi kati yao. Kila mmoja anamnyoshea kidole cha hasira  mwenzake na kusema, “OLE WAKO MIMI NIFUKUZWE SHULE,NITAKUFA NA MTU
Neno la mwisho  nililoweza kulisikia toka kwa baba yangu ni hili, “Wee binti, ambaa upesi na tawanyika hapa, usinijue mimi tangu leo wala kunibughudhi, wala usinifanyie uchuro. Ondoka kwangu we Fisi jike na kongwe. Aliyekwambia hiyo mimba ni ya kwangu nani? Mimi kwanza sikujui kabisa! Umekuwa kiruka njia kwa kila mvulana hapa shuleni na sasa unataka kunitupia mimba zao mimi? Eboo! pole sana binti! imekula kwako hiyo!”.
Hapo mama yangu alitoka anapepesuka kama amelewa, ananawa machozi usoni huku akijisemea peke yake, “Sitaki sitaki, hata mimi sitaki hili toto lako. Loo! nifukuzwe shule kwaajili yako! Hapana hapana! Mtoto(mimi) nitamtunzaje na shule nikifukuzwa na bila shaka sote tutafukuzwa. Na wazazi wangu bado hawajui. Wakijua nitaingia nyumba ya nani?”
          Basi niliona mama yangu anarudi kwa yule mganga na kuomba aitoe ile mimba yaani aniue mimi. Mganga alidai za mchuzi. Hapo niliona mama yangu anafungua pochi yake na kuchomoa noti chache na kumpa yule mganga. Naye alizipokea haraka na kuweka mfukoni. Hapo sasa hata mimi nilianza kuona damu yangu inanuka mdomoni mwangu. Yule mganga alichukua dawa fulani, niliweza kusoma jina la dawa ile, chupa yake ilikuwa   imeandikwa `Salt Poisoning` Akaitia ile dawa katika sindano, naye akaichomeka ile sindano katika mwili wa mama yangu na kuiminya ile sindano, nayo dawa ikaanza kusogelea kitovuni pangu polepole. Kama ujuavyo kile kitovu ndio njia yangu maalumu ya kupatia chakula changu toka kwa mama yangu.
          Aaaah! Dawa ile!! Dawa ile jamani!! Kweli kabisa dawa ile! Bado toka kaburini ninaikumbuka sana dawa ile `salt Poisoning`. Ilishuka polepole tumboni mwa mama yangu kadiri yule mganga alivyoiminya ile sindano, ilishuka kama kisu kikali sana kinachonisogelea kutaka kunichinja na kunichanachana  kama vipande vya nyama ya kuchoma mshikaki. Hatimaye iliingia kitovuni pangu na kupenya mwili wangu mzima kwa njia ya damu yangu. Jamani! Jamani! mmh, kwanini lakini mama kuniua?
 Mara nilianza kupiga chafya, kutaka kulia nikashindwa, kukimbia pia nisiweze, kusema nako nikashindwa. Mwili wote ulikuwa wa moto kabisa. Viungo vyangu vyororo vilianza mara kuchanika na kunyong`onyea vyote kabisa. Mifupa yangu ikaanza kusagika kama mchanga na mwili wangu kuyeuka kama nta ya mshumaa na kuwa kama uji.
Jamani! Jamani! Mnionee huruma mwenzenu. Niliwatazama kwa huruma yule mganga na mama yangu wanavyonichakaza maskini mimi, mtoto wa mtu. Nilivuruguta na kusononeka na kumtazama mama yangu kwa macho ya huruma na maombolezo, lakini alikunja uso wake kabisa na hakunijali,nami nisimwone mtu wa kunisaidia.
          Mara mikono yangu ilitupwa huku na miguu kule, tumbo huko, kichwa changu huko na matumbo yangu yakakunjuka kama kamba. Macho yangu yalinitoka nje pima.
Ndipo nilipotoa pumzi yangu ya mwisho masikini, kuitoa roho yangu yenye huzuni na majonzi tele na mkato wa tamaa wa kuishi tena hapa duniani. Jamani! Kweli watu wema hawana maisha marefu hapa duniani!
NDIPO PAMOJA NA AYUBU NA NABII YEREMIA NILIPOFUNUA KINYWA CHANGU NA KUILANI SIKU NIKIYOTUNGIKA MIMBA!!
Baada ya hayo yote kunisibu, ndipo nilipofunua kinywa changu nakuilaani siku ile  yangu ya mkasa, nikisema “Na ipotelee mbali ile siku niliyotungika mimba mimi. Isibarikiwe siku ile niliyotungika mimba na wazazi wangu.
            Siku ile na iwe giza daima. Siku ile na Mungu asiiangalie toka mbinguni. Siku ile wala mwanga wa jua usiiangazie. Ishikwe na giza tupu, wingu na litandwe juu yake. Tena usiku  huo, na ushikwe  na giza  kuu, usihesabike katika siku za miaka, wala kutiwa hesabu ya miezi. Nawalaani hao walaanio mchana. Tazama usiku huo daima uwe tasa wala ndani yake msiwe na sauti ya shangwe. Siku hiyo sitaisahau maishani mwangu. Sasa nafahamu vizuri sana kwanini saa ile Yesu alilia pale juu ya msalaba, “Mungu wangu! Mungu wangu! Mbona umeniacha? Nami siku ile nililia kwa huzuni kali “Mama yangu! mama yangu!  Mbona unaniua? Jamani! Kifo ni kichungu, si cha kuombea kikufike, omba jingine.

ΓΌ KILIO CHANGU TOKEA KABURINI

Toka kaburini naendelea kujiuliza, wala jibu toka kwa Mama yangu sipati wala toka kwa watu wengine sipati.
          Baada ya mganga kuingiza koleo tumboni kwa mama yangu alianza sasa kunyofoa na kutupa nje mifupa yangu yote na nyama ya mwili wangu akatumbukiza kwenye lindoo fulani bovu! Halafu mganga akamwambia Mama yangu, haya sasa tayari, toa nje na kutupa jalalani au fukia. Mama yangu aliichukua ile ndoo mbovu, yenye vipande vya mwili wangu akaendanayo porini kidogo, akachimba pale shimo dogo, hapo akamwaga mwili wangu akaufukia.
Jamani kilio changu mwenzenu kinatoka bado pale udongoni aliponifukia Mama yangu mpenzi. Pale mpaka sasa bado mwili wangu unapumzika kungojea  hukumu yangu siku ya kiama.
Enyi mnaopita karibu na kaburi langu, naomba kujiuliza kwenu wenzangu nifahamu; Mliwatendea nini mama zenu mlipokuwa kama mimi hata wakawahurumia wasiwaue? Mbona hamkuweza kusema kama mimi, kulia kama mimi, kujitetea kama mimi? Au mliwafurahishaje mama zenu, mbona mwenzenu leo nauawa na mama yangu tangu tumboni mwake? Nanyi wenzangu mliouawa na kutupwa chooni au porini kama mimi, njooni tumlilie Mungu, kilio chetu cha maombolezo. Abel alimkosea nini Kaini? Watoto mashahidi waliochinjwa bure na Herode wakati wa Yesu walikosa nini? Kosa langu hasa lilikuwa ni nini? Jamani mimi sikuwachagua wazazi, sikuwalazimisha wanilete duniani, wala sikuwaomba siku ile wakutane pale kichakani. Mama yangu mpenzi, mimi nilikukosea nini?Tabasamu na pendo langu kwako nilivyoviandaa kukutolea mara baada ya kuzaliwa kwangu, nawe kwa hili unalilipa kwa kifo cha uchungu namna hii Mama!! Ulikubali ile dawa inisagesage na kunirarua mifupa yangu yote kama simba katili anayerarua nyama yangu, mimi ningali tumboni mwako. Nililia na kutoka machozi saa ile, nawe ukaziba masikio yako. Nilikutazama kwa huzuni sana usoni, lakini ukanifumbia macho mwanao.
          Tumbo lako lilipokuwa linakusokota, baada ya kuchomwa ile sindano, ni mimi niliyekuwa nayeyuka, nanyumbuka viungo vyangu na kusononeka kwa uchungu sana Mama. Je, Wewe leo kama mama yako asingekutetea ulipokuwa hujiwezi kama mimi leo ungekuwa wapi mama? Je, ulimtendea jema gani mama yako tumboni mwake hata ukamfurahisha asikuue? Kuniua mwanao niliyekupenda kwa moyo wangu wote! Kuniua mwana wa tumbo lako mwenyewe! tena mwana wako mzaliwa wako wa kwanza? Mama mpenzi, huko ndiko kunipenda kweli mtoto wako na kunitakia heri ya kweli kwa kunifungia hata mlango wa Mbinguni, yaani bila hata kubatizwa, kweli mama yangu? Hebu fikiria mama  yangu unataka mimi niende wapi na hata nifanye nini bila kuishi na Mungu? Ni kweli mama yangu hutaki hata nimrudie Mungu wangu aliyeniumba kwa sura na mfano wake? Mama, Mama yangu! kumbuka kuwa machozi yangu yanaanguka kifuani mwangu na kutiririka kifuani mwako wewe mama yangu. Damu yangu Mama, kumbuka ni yako mwenyewe, uliyoamua kuimwaga bure. Ule mwili wangu ulioutupa pale udongoni,ni mwili wenu ninyi wazazi wangu uliotokana na ulevi wenu siku ile.
Mbali na kuwa nimekosewa haki zangu zote za kuishi kama binadamu hapa duniani, bado kilio changu na damu yangu vinamlilia Mungu wangu. Kama vile damu ya Abeli na wengine, ambao damu yao isiyo na hatia yoyote ilimwagwa na bado inaendelea kumwagwa hapa dunia. Damu hizo zote bado zinamlilia Mungu toka pale udongoni. Mungu wangu, ingawa wazazi wangu wamenitupa, tafadhali sana nakuomba, Baba, wewe usinitupe milele. Mimi ni mtoto wako, ingawa sistahili kuitwa hivyo. Baba pokea roho yangu uliyoiumba kwa sura na mfano wako Mungu. Leo nairudisha roho yangu mikononi mwako Baba. Najua Mama yangu ameniua mimi mwanae sababu ya ubinafsi wake, ili yeye aendelee na shule na kujifurahisha na anasa za dunia hii. Na ndio maana hakujali  kuniua mwanae mzaliwa wake wa kwanza niliyempenda sana.
          Haya, kwaheri mama yangu! Tutaonana mbele ya safari panapo majaaliwa. Nawaombea msamaha na Baba yangu Anton huko shuleni aliko.Nadhani naye sasa amejifunza kitu, kwamba maisha ya kudanganyana yanamadhara. Naomba Mungu asilihesabu kosa lao hili siku ya kiama.
Namaliza kwa kusema kuwa...


ASANTE MGANGA KWA KUTUMIA UTALAMU WAKO KUUA WANYONGE. LAKINI SIKU YA KUPEWA KAZI HII SI ULIAPA KUWA KUUA KWAKO NI MWIKO!?

ASANTE BABA KWA KUNILETA MWANAO DUNIANI KWA MCHEZO TU NA ULEVI!.

ASANTE SANA MAMA YANGU, NI MIMI MWANAO NAKUSALIMU, SHIKAMOO!KILA UKIPITA PALE KICHAKANI, DAIMA KUMBUKA KUWA MIMI MWANAO BADO NIPO PALE ULIPONIFUKIA SIKU ILE!


~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Simulizi hii iliwahi kutolewa katika Gazeti la MWENGE mwaka 2013
Hivi punde simulizi hii itawekwa kwa mtindo wa sauti ikirekodiwa kupitia Precious Records.

Ahsanteni

1 comment:

  1. Baada ya kuwa na uhusiano naye kwa miaka saba, aliachana nami. Nilijaribu kila niwezalo kumrudisha lakini yote yalikuwa bure. Nilitamani arudi vibaya sana kutokana na mapenzi niliyonayo kwake na nilimsihi kwa moyo wangu wote, nilimpa ahadi lakini alikataa. Niliwasiliana na mganga aitwaye DR Dawn, ambaye angeweza kunisaidia kuniroga ili kumrejesha lakini mimi ni mtu ambaye sikuwahi kuamini uchawi, sikuwa na jinsi zaidi ya kujaribu. Nilimtumia barua pepe mganga huyo na akaniambia kwamba hakuna tatizo lolote, kwamba kila kitu kitakuwa sawa baada ya siku mbili na kwamba mpenzi wangu wa zamani angerudi kwangu baada ya siku tatu. Alipiga uchawi na cha kushangaza, siku ya pili, ilikuwa karibu 4:00 PM. Mpenzi wangu wa zamani alinipigia simu, tukasuluhisha tofauti zetu na sasa tuna furaha pamoja. Yeyote anayeweza kuhitaji usaidizi wa mtangazaji huyo anaweza kumtumia barua pepe kwa ( dawnacuna314@gmail.com ) au /WhatsApp kwa: +2349046229159

    Kwa uchawi wa kuungana tena.
    Kwa ujanja wa ujauzito.
    Kushinda bahati nasibu.
    Kushinda kesi mahakamani.
    Mimea ya kutibu, kila aina ya magonjwa kama,
    VVU UKIMWI Kansa malengelenge na zaidi.

    ReplyDelete

NITAKUPENDA DAIMA

Mtunzi: Elias Kalistus Mwalongo Chuo Kikuu Cha Kikatoliki Ruaha(RUCU) Simu: 0769313224 ____________ Laazizi wangu wa moyo, nat...